THE BEST BLOG IN TOWN

Powered by Blogger.

Text

RSS

Akamatwa akitengeneza silaha kienyeji

24th July 2013


Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata majambazi wanane akiwamo mmoja ambaye amebainika kumiliki kiwanda cha kienyeji kinachotengeneza silaha. Jeshi hilo limemtaja mtuhumiwa anayemiliki kiwanda hicho kuwa ni Charles Masunzu (30), ambaye ni Msukuma na mkazi wa Kawe Mzimuni, jijini Dar es Salaam. Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kaimu Kamishna wa Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Ally Mlenge, alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa na silaha mbalimbali ambazo ni rifle tatu, risasi 36, pingu, mitutu mitano iliyotengenezwa kienyeji, Shortgun, mfuko wa kuhifadhia silaha na maganda 17. Vitu vingine alivyokutwa navyo ni Pistol KJW works, cocking handle za silaha, ‘house’ ya silaha aina ya Greenel, Magazine iliyounganishwa na tiger guard ya silaha ya aina ya riffle, shortgun moja namba 2539 double bore na vikato vitatu vya silaha. Aidha vifaa vingine ni meza moja yenye vice clamp kwa ajiri ya kutengenezea silaha kienyeji, mikasi minne ya aina tofauti, mipini mitatu ya silaha aina ya riffle, funguo mbalimbali, nyundo, makufuli, misumeno ya kutengeneza vyuma na vielelezo vingine vinavyohusiana na uhalifu. Mtuhumiwa alikiri kuhusika na matukio mbalimbali ya unyang’anyi na kusababisha mauaji mengi sehemu mbalimbali. Jambazi huyo ameshikiliwa na jeshi la polisi na atafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika. Aidha, Jeshi la Polisi linawashikilia majambazi wanne waliokutwa na bunduki aina ya SMG iliyosajiliwa kwa namba 02704 ikiwa na risasi 20 ndani ya magazine yake na ikiwa imekatwa kitako. Baada ya mahojiano na jeshi la polisi, majambazi hao walikiri kujihusisha na matukio ya uporaji na kwamba bunduki hiyo walimpora askari polisi Wilaya ya Rufiji akiwa anasindikiza magari kutoka Ikwiriri Mkoani Pwani mnamo mwaka 2007. Kadhalika, jeshi hilo lilifanikiwa kumkamata tapeli aliyejulikana kwa jina la Mfaume Omari (29) mkazi wa Magomeni Kagera, aliyekuwa akitumia majina ya viongozi wa serikali, viongozi wa dini na watu maarufu kujipatia fedha kwa kuvaa uhusika wa majina hayo. Mlenge alisema, baada ya kufuatilia nyendo za mtuhumiwa, jeshi la polisi lilipata taarifa kutoka kwa Mchungaji Getrude Rwakatare kuwa jina lake lilikuwa likitumiwa vibaya na mtuhumiwa huyo. Aidha jeshi la polisi lilifanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo akiwa anamiliki simu yenye namba 0659 736 454 ikiwa imesajiliwa kwa jina la Mfaume Saidi Omari na 0659 164 744 ikiwa imesajiliwa kwa jina la Alex Mtenga.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Mwanasheria Mkuu awaasa wanasheria kuepuka rushwa

24th July 2013


Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Frederick Werrema

Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Frederick Werrema, amewaasa wanasheria nchini kutojihusisha na vitendo vya rushwa wawapo katika majukumu yao ya kazi. Werrema alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam wakati akifungua semina ya wanasheria wapya wa serikali ambao baada ya mafunzo hayo ya muda mfupi kuwajengea uwezo wanatarajiwa kupangiwa vituo vipya vya kazi. Aliwataka wanasheria hao wapatao 30 kuzingatia maadili ya taaluma yao pamoja, kutenda haki na kujiepusha na vitendo vya rushwa ili kupotosha hukumu. Kauli ya Werema inakuja huku wimbi kubwa la ufisadi kama vile rushwa likielezwa na watafiti mbalimbali kuvifunika vyombo vya dola ikiwamo mahakama, polisi na vituo vya afya. Hivi karibuni Shirika la Utafiti la Kimataifa la Transparency la nchini Kenya, lilitoa takwimu za vitendo vya rushwa kushamiri katika maeneo hayo ya dola kwa nchi takribani 120. Baadhi ya nchi zilizoonekana kukithiri kwa vitendo hivyo vya kifisadi ni pamoja na Uganda na Tanzania.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS